RT Kuwabana Waandaaji wa Mbio

August 20, 2025


WhatsApp%20Image%202025-08-20%20at%2015.09.17


SHIRIKISHO la Riadha Tanzania (RT) limepanga kuweka sheria mpya itakayowalazimisha wandaaji wa mashindano kuhakikisha wanajumuisha pia mbio za watoto katika kila tukio litakaloandaliwa.


Hatua hiyo inalenga kujenga msingi imara wa vipaji na kuwekeza mapema kwenye maendeleo ya riadha nchini.


Rais mpya wa RT, Rogath John Stephen Akhwari, alisema mpango huo utahusisha kuandaa mashindano maalumu ya watoto na vijana kwa kila kanda, yakiratibiwa kwa kushirikiana na vyama vya mikoa ili kuhakikisha kunakuwepo mtiririko wa mashindano kuanzia ngazi ya chini.


Akhwari alibainisha kuwa wapo mbioni kuandaa kanuni mpya za kusimamia mbio za barabarani, ambapo kutakuwa na utaratibu wa kutofautisha mashindano ya kimaifa yatakayosimamiwa na RT moja kwa moja na yale ya ndani yenye malengo ya kitaifa, kwa lengo la kuongeza ubora na hadhi ya riadha nchini.


“Hizi mbio itakuwa ni lazima, siyo chaguo tunataka kuboresha kanuni zetu na yeyote atakayehitaji kibali cha kuandaa mashindano atalazimika kuhakikisha mbio za watoto pia zitakuwepo,” alisema Akhwari.


Alieleza watapeleka wataalamu waliobobea ili kusaidia wandaaji kuelewa namna sahii ya kuandaa mashindano ya watoto, akisisitiza kuwa changamoto kubwa iliyokuwepo awali ni watoto kukimbia mbio ndefu zisizolingana na umri wao.


"Watoto wetu wamekuwa wakikosa fursa hizi, kwa sababu mara nyingi wakipewa mbio wanakimbizwa umbali wa kilometa tano, hapo awali tulivumilia kwa sababu tulikuwa hatuna mfumo madhubuti lakini sasa tunataka kubadilisha hilo,” aliongeza.


Aidha kabla ya sheria mpya kupitishwa, RT imesema itatoa elimu kwa wandaaji wote wa mbio, kisha kuwapa muda wa maandalizi kabla ya utekelezaji rasmi.


Akhwari anasema hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa muda mrefu wa kuhakikisha riadha Tanzania inakua kwa kuanzia watoto, vijana hadi kuzalisha wanariadha wa kiwango cha kimataifa.


Imeandaliwa na Mwananchi Communications Limited

MAPOKEZI YA RAIS WA RT ROGATH JOHN STEPHEN AKHWARI JIJINI ARUSHA

August 18, 2025

 

Kocha Mwingereza akimpongeza rais wa shirkisho la Riadha Tanzania -RT Kocha Rogath John Stephen Akhwari wakati wa mapokezi katika uwanja wa Kumbukumbu ya Sheikh Amri Abeid Jijini Arusha Leo.

Mke wa Rogath John (katikati mwenye jaketi jekundu) akimpongeza mume wake kwa kuchaguliwa kuwa rais wa shirikisho la Riadha Tanzania -RT wakati wa mapokezi katika uwanja wa Kumbukumbu ya Sheikh Amri Abeid Jijini Arusha Leo.
Rais wa shirikisho la Riadha Tanzania -RT Kocha Rogath John Stephen Akhwari Akiwashukuru Watanzania wote kwa Kumuombea na hatimaye kuchaguliwa kuwa rais , pia amechukua nafasi hiyo kumshukuru Rais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mchango wake kwenye michezo.


Na John Mhala, Arusha.

ARUSHA: Rais wa Shirikisho la Riadha Tanzania (RT) Rogath John Stephen Akhwari amesema safari ya kuendeleza mchezo wa riadha ndio imeanza kwani shirikisho hilo litaanzisha rasmi mbio za watoto na vijana lengo ni kuwatayarisha wenye umri huo kuwa kurithi mikoba ya wanariadha wanaojiandaa kustaafu.

Stephen amesema hayo leo alfajiri alipowasili jijini Arusha akitokea Mwanza baada ya kuchaguliwa na wajumbe wa RT kuwa Rais wa Shirikisho hilo na kusema kuwa wakati umefika sasa wa kuwaandaa watoto na vijana kushiriki mchezo wa riadha ili waweze kushika nafasi za akina Alphonce Simbu ,Magdalena Shauri,Jackline Sakilu na Gabriel Geay watakapostaafu.

Amesema RT lazima ijiandae kwa kuwaanda watoto na vijana ili waupende mchezo huo na hatimaye waweze kufanya vizuri kitaifa na kimataifa ikiwa ni pamoja na kushika zile nafasi walizofanya vizuri wanariadha wenzao hivyo wale wote wanaoanzisha na walioanzisha mbio kote nchini kipaumbele ni kuanzisha mbio za watoto na vijana mara moja kwani ndio lengo la msingi la kukuza mchezo huo unapendwa kwa sasa hapa nchini.

Rais huyo amesema ajira kwa sasa ni ngumu iwe ndani ya serikali na nje ya serikali na ajira nzuri ni mchezo wa riadha hivyo aliwaasa wazazi kuwapa ushirikiano watoto na vijana kujikita katika mchezo huo kwani una pesa nyingi kwa muda mfupi na kutoa mfano Simbu aliposhinda mbio za Boston amepata fedha nyingi ambazo hata waziri akistaafu serikali hawezi kuzipata.

Rogath ambaye mwajiriwa wa jeshi la Polisi nchini na kituo chake cha kazi Polisi Kati Arusha kwa cheo cha Mrakibu Msaidizi Mwandamizi (ASP) alimshukuru sana Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini (IGP) Inspekta General wa Polisi, Camilius Wambura kwa kumpa baraka za kuchukua fomu za kuwania kinyang’anyanyiro hicho na hatimaye kushinda urais.

CRDB BANK MARATHON YAFANYIKA DAR

August 17, 2025


Dar es Salaam, 17 Agosti 2025 - Maelfu ya wakimbiaji na wapenda michezo kutoka ndani na nje ya Tanzania wamejitokeza leo katika viwanja vya The Green, Oysterbay, kushiriki CRDB Bank Marathon 2025, mbio za hisani ambazo mwaka huu zimekusanya Shilingi Bilioni 2 ili kusaidia matibabu ya watoto wenye matatizo ya moyo, wakinamama wenye ujauzito hatarishi, na vijana kupitia programu ya iMBEJU.
Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Tulia Ackson Mwansasu, aliongoza maelfu ya washiriki kwenye msimu huu wa sita wa CRDB Bank Marathon. 
Akitoa salamu zake, Dkt. Tulia alipongeza ubunifu wa CRDB Bank Foundation katika kuunganisha jamii kupitia michezo na kusaidia wenye uhitaji, akieleza kuwa mbio hizo ni mfano wa vitendo vya huruma vinavyogusa maisha ya wengi. 
 
“Ushiriki wetu katika CRDB Bank Marathon ni tendo la huruma linaloleta faraja kwa watoto na wakinamama na familia zao. Ni ushahidi kwamba tukishirikiana, tunaweza kubadilisha maisha,” alisema.
Akitoa salamu zake, Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi, aliipongeza Benki ya CRDB na CRDB Bank Foundation kuendelea kuandaa mbio hizo. 
 
Alisema, “CRDB Bank Marathon si tu imekuwa ikikuza afya na mshikamano wa kijamii, bali pia imekuwa ikifungua milango ya ajira na fursa za kiuchumi kwa vijana wetu. Michezo ni sekta inayoweza kubadili maisha, na ninapongeza sana kitendo cha kuweka zawadi nono kwa washindi. Hizi ni fursa ambazo zinaweza kuwa mtaji wa kuanzisha biashara na kuimarisha maisha ya vijana wetu. Serikali itaendelea kushirikiana na wadau kama CRDB Bank Foundation kuhakikisha michezo inakuwa chachu ya maendeleo ya taifa.”
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela, alibainisha kuwa msimu wa sita wa CRDB Bank Marathon umefanyika sambamba na maadhimisho ya miaka 30 ya Benki ya CRDB, na kuendelea kupanua wigo wa matokeo yake ndani na nje ya Tanzania. Kwa mara ya pili, mbio hizi zimefanyika pia nchini Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), zikikusanya fedha kwa ajili ya miradi ya afya na ustawi wa jamii katika nchi hizo. 

Nsekela alisema kuwa mbio za mwaka huu zimeweza kuvutia zaidi ya washiriki 16,000, na kufanikisha lengo la kukusanya shilingi bilioni 2 ambapo pamoja na kusaidia maandalizi ya mbio hizo, shilingi milioni 450, zimeelekezwa kusaidia wenye uhitaji katika jamii. 
 
Kati ya hizo shilingi milioni 100 zimekwenda hospitali ya CCBRT kusaidia wakinama wenye ujauzito hatarishi kujifungua salama, shilingi milioni 100 zimekwenda Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) kusaidia upasuaji wa Watoto wenye matatizo ya moyo, na shilingi 250 zitaelekezwa katika uwezeshaji wa vijana.
Akizungumza wakati wa kutangaza matokeo ya mbio hizo, Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Bank Foundation, Tully Esther Mwambapa, alieleza kuwa safari ya msimu wa sita imeanzia Lubumbashi, DRC, ambako zilikusanywa Dola za Marekani 70,000 kwa ajili ya kuboresha huduma za afya katika hospitali ya Jeshi la Ruashi, na kuendelea Bujumbura, Burundi, ambapo zilipatikana Faranga za Burundi milioni 175 kusaidia bima ya afya kwa zaidi ya watu 58,000 wasiojiweza. 
 
Mwambapa alisisitiza kuwa mafanikio haya ni matokeo ya mshikamano wa kipekee wa serikali za nchi shiriki, wadhamini na washiriki, akiwashukuru wadau wote waliotoa jitokeza kuchangia ikiwamo kampuni za bima za Sanlam Life na Alliance Life ambao wamekuwa sehemu ya mbio hizi tangu kuanzishwa kwake.
Washindi wa mbio za mwaka huu upande wa Tanzania kwa Kilometa 42 upande wa wanawake ni Joyloyce Kemuma kutoka Kenya, upande wa wanaume mshindi ni Abraham Kiptum kutoka Kenya. Kilometa 21 upande wa wanawake ni Catherine Syokau kutoka Kenya, na upande wa wanaume ni Joseph Panga kutoka Tanzania. Kilometa 10 upande wa wanawake ni Silia Ginoka kutoka Tanzania, na upande wa wanaume ni Boayi Maganga kutoka Tanzania.
 
Joseph Panga mshindi wa mbio za Kilometa 21 upande wa wanawake ameeleza furaha yake kushiriki katika mbio hizo na kusema kuwa ushindi wake ni sehemu ya kusaida matibabu ya watoto wenye matatizo ya moyo na matibabu ya wakinamama wenye ujauzito hatarishi hospitali ya CCBRT. 
 
“Mimi kama Mtanzania najisikia fahari kubwa kushiriki kusambaza tabasamu kwa watoto na wakinamama. Ni muhimu watu kufahamu kuwa afya bora ni haki ya kila mtoto, na hakuna mama anayestahili kupoteza maisha wakati wa kujifungua. Tunawashukuru CRDB Bank Foundation kwa kutuleta pamoja katika harakati hizi za kuokoa maisha,” amesema.
CRDB Bank Marathon imekuwa jukwaa muhimu la kuchochea ustawi wa kijamii katika ukanda huu wa Afrika ya Mashariki na kati hivi karibuni ikipata heshima ya kutambuliwa kimataifa kwa kushinda tuzo ya jukwaa bora la taasisi za fedha katika kusaidia kusaidia jamii.

ROGATH JOHN STEPHEN AKHWARI ACHAGULIWA KUWA RAIS WA SHIRIKISHO LA RIADHA TANZANIA

August 17, 2025

 

Kocha wa Polisi Tanzania na Katibu Mkuu wa Riadha Chama cha Mkoa wa Arusha Rogath John Stephen Akhwari amechaguliwa na wajumbe kuwa Rais wa Shirikisho la Riadha Tanzania huko Mwanza tarehe 16/08/2025 kwa kupata Kura 27 kati ya 47 na mpinzani wake Bw. Nsolo Malongo Mlozi kupata kura 20. 
Wakili Jackson Beda Ndaweka Achaguliwa kuwa Makamu wa Shirikisho la Riadha Tanzania -RT , baada ya kuitumikia shirikisho la riadha Tanzania kama Kaimu Katibu Mkuu kwa Muda mrefu.

 

Copyright © 2015 - 2025 Athletics Tanzania All Right Reserved

Developed by Gadiola Emanuel
Theme By AP | Developed By Gadiola Emanuel