Waziri Maghembe 'kuibeba' Rock City Marathon

August 22, 2017





Dar es Salaam;WAZIRI wa Maliasili na Utalii Prof Jumanne Maghembe mwishoni mwa wiki hii alizindua rasmi usajili wa msimu wa nane wa mbio za Rock City Marathon huku akiahidi kushirikiana na waandaaji wa mbio hizo katika kuhakikisha kuwa zinatumika vema kuutangaza utalii wa ndani.


Akizungumza kwenye hafla fupi ya uzinduzi huo iliyofanyika katika Hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na wadau mbalimbali wa mchezo huo wakiwemo viongozi wa serikali pamoja na wadhamini mbalimbali wa mbio hizo, Waziri Maghembe alisema azma yake hiyo inasukumwa na malengo ya mbio hizo ambayo ni kutumia mchezo wa riadha katika kutangaza utalii hususani katika Ukanda wa Ziwa.


"Kwa kuzingatia uzito wa malengo ya mbio hizo nitamke bayana kuwa nipo tayari kushirikiana na waandaaji wa mbio hizi kuhakikisha kwamba kuanzia mwaka huu mbio hizi zinafana na zinavutia washiriki wengi zaidi hususani wa kimataifa,'' alisema Waziri Maghembe ambae pia alithibitisha ushiriki wake kwenye mbio hizo zinazoratarajiwa kufanyika Octoba 29, mwaka huu kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza na kupita katika barabara mbalimbali za jiji hilo kabla hazijamalizikia katika uwanja huo.


Mbali na ushiriki wake,Waziri Maghembe alitoa wito kwa mashirika mbalimbali yaliyo chini ya wizara yake ikiwemo la Hifadhi za Taifa(Tanapa), Mamlaka ya Usimamizi Wanyamapori (TAWA), Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA), Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) na Makumbusho ya Taifa kuhakikisha wanashiriki kikamilifu katika kufanikisha mbio hizo.


"Ukanda wa Ziwa una vivutio vingi ambavyo pia kama Wizara yenye dhamana ya utalii lazima tuvigeukie na kuvitangaza kwa nguvu na kwa njia tofauti ikiwemo michezo,'' alisema Waziri Maghembe huku akivitaja baadhi ya vivutio hivyo kuwa ni pamoja na Kisiwa cha Saanane, Makumbusho ya kabila la Wasukuma pamoja na tamaduni za makabila ya wakazi wa Kanda ya Ziwa.


Mbio za Rock City Marathon zilizoanzishwa miaka minane iliyopita zinazozidi kujiongezea umaarufu kila mwaka na tayari zimefanikiwa kuwavutia baadhi ya wadhamini ikiwa ni pamoja na kampuni za TIPER, PUMA, Bodi ya Utalii Tanzania (TTB),Mwanza Hotel , Real PR Solutions Limited, Afrimax Strategic Partnerships Limited, EF Outdoor, CF Hospital na ATCL.


Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya mbio hizo, Bw Zenno Ngowi alitoa wito kwa washiriki wa ndani hususani wa mikoa ya Kanda ya Ziwa pamoja na wadhamini kujitokeza kwa wingi kushiriki katika mbio hizo ambazo kwa mwaka jana zilifanikiwa kuhusisha washiriki zaidi ya 2000 na watazamaji zaidi ya 30,000.


Naye Mratibu wa mbio hizo zinazoandaliwa na kampuni ya Capital Plus International, Bi Adeline Ndesanjo alisema mbio za mwaka huu zinatarajiwa kuhusisha washiriki wengi zaidi kutoka kila kona ya dunia ikiwemo Afrika, Ulaya,China,Mashariki ya Kati hususani Israel na Marekani huku akitoa wito kwa washiriki wa ndani kujisajili kwa wingi ili kuthibitisha ushiriki wao kwenye mbio hizo.


Akizungumza kwa niaba ya wadhamini wengine wa mbio hizo Meneja Masoko wa Kampuni ya mafuta ya Puma, Bw Machumani Shebe alisema ushiriki wao umechagizwa zaidi na azma ya kampuni hiyo kuisaidia serikali katika kuutangaza utalii wa ndani.


"Tukiwa kama wadau muhimu katika biashara ya mafuta hususani mafuta ya ndege tunategemea sana ustawi wa sekta ya utalii katika kuongeza soko la biashara yetu na kwa kuwa mchezo wa riadha umekuwa ukitumika zaidi katika kuwavutia watalii tukaona kuna haja ya kuunga mkono ufanikishaji wa mbio hizi,'' alisema.




WAZIRI wa Maliasili na Utalii Prof Jumanne Maghembe akizungumza na wadau mbalimbali wa mchezo wa riadha hapa nchini pamoja na waandaaji wa mbio za Rock City Marathon kwenye hafla maalumu ya uzinduzi rasmi usajili wa msimu msimu wa nane wa mbio hizo iliyofanyika mwishoni mwa wiki jijini Dar es salaam.

Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya mbio hizo, Bw Zenno Ngowi akizungumza kwenye hafla hiyo. Alitoa wito kwa washiriki wa ndani hususani wa mikoa ya Kanda ya Ziwa pamoja na wadhamini kujitokeza kwa wingi kushiriki katika mbio hizo ambazo kwa mwaka jana zilifanikiwa kuhusisha washiriki zaidi ya 2000 na watazamaji zaidi ya 30,000.

Mratibu wa mbio hizo zinazoandaliwa na kampuni ya Capital Plus International, Bi Adeline Ndesanjo akitoa maelezo kuhusu maandalizi ya mbio hizo kwenye hafla hiyo. Alisema mbio za mwaka huu zinatarajiwa kuhusisha washiriki wengi zaidi kutoka kila kona ya dunia ikiwemo Afrika, Ulaya,China,Mashariki ya Kati hususani Israel na Marekani .

Wadhamini nao hawakuwa nyuma!Meneja Masoko wa Kampuni ya mafuta ya Puma Energy, Bw Machumani Shebe alisema ushiriki wao kwenye mbio hizo umechagizwa zaidi na azma ya kampuni yake hiyo kuisaidia serikali katika kuutangaza utalii wa ndani.


Baadhi ya wageni waalikwa waliohudhuria hafla hiyo.


WAZIRI wa Maliasili na Utalii Prof Jumanne Maghembe akiwa kwenye picha ya pamoja na waandaaji wa mbio hizo pamoja na wadau mbalimbali wa mchezo huo wakiwemo viongozi wa serikali pamoja na wadhamini wa mbio hizo.

WATANZANIA KUTIMUA VUMBI LONDON LEO! KUONEKANA MBASHARA DStv

August 05, 2017






Timu ya Taifa ya Riadha inayoshiriki mashindano ya Dunia ya riadha yanayoendelea jijini London inaanza kibarua cha kuipeperusha bendera yetu leo (Jumamosi 05/08/2017) ambapo mfukuza upepo Failuna Abdi Matanga atakimbia mbio za mita 10,000 leo .


Failuna atashuhudiwa na maelfu ya watanzania kupitia DStv Muda wa saa mbili usiku.

Akithibitisha kuonekana kwa matangazo hayo kupitia DStv, Mkurugenzi Mtendaji wa Multichoice Tanzania Maharage Chande amesema DStv imefanya jitihada kubwa na kuhakikisha kuwa watanzania wanaishuhudia timu yetu ikituwakilisha katika mashindano hayo muhimu ulimwenguni.

“Tunawahakikishia watanzania burudani hii moja kwa moja kupitia DStv chaneli za Supersport. Tunaamini sote tutakuwa nyuma yao wachezaji wetu kuwashuhudia jinsi wanavyotuwakilisha” alisema Maharage

“Suala la watanzania kuwashuhudia vijana wetu wakishiriki katika mashindano makubwa kama haya lina maana kubwa sana. Vijana wadogo wakiwaona dada zao na kaka zao wakishiriki mashindano makubwa kama haya inawatia moyo na kuwapa ari na tamaa ya wao kujitahidi na kufika hatua kama hizo. Hili ni jambo la muhimu sana na sisi DStv tunalitilia mkazo sana. Ni njia moja wapo ya kuwashawishi na kuwatia moyo vijana wetu wanaochipukia na kuwajengea kujiamini”

Baada ya Failuna anayekimbia mita 10,000, watanzania watashuhudia tena shughuli pevu siku ya jumapili kupitia DStv kuanzia majira ya saa nne asubuhi ambapo vidume watatu - Alphonce Felix Simbu, Ezekiel Jafari Ng’imba na Stefano Huche Gwandu watakuwa wakikata upepo katika viunga vya jiji la Malkia London ikiwa ni mbio ndefu za kilomita 42.

Baada ya vidume hao kukamilisha kazi tuliyowatuma, wanawake wetu wa shoka nao wataingia barabarani ambapo Tanzania inawakilishwa na Sara Ramadhani Makera na Magdalena Crispin Shauri ambao nao watafukuza upepo umbali wa kilomita 42 majira ya saa nane mchana. Patashika yote hii itaonekana DStv.

Wanariadha wengine wawili wa mbio fupi za mita 5,000 ambao ni Emmanuel Giniki Gisamoda na Gabriel Gerald Geay watatimka siku ya Jumatano tarehe 9 Agosti majira ya mbili usiku hii ikiwa ni raundi ya mchujo na wakifuzu watashiriki fainali ya mita 5,000 siku ya Jumamosi Agost 12, majira ya mbili usiku. Nao pia watashuhudiwa mbashara kupitia DStv

Mashindano ya Dunia ya Riadha yalianza rasmi 1983 ambapo Tanzania imewahi kupata medali 1 tu ya Fedha kupitia mwanariadha Christopher Isegwe kwenye mbio za Marathon 2005 Helsinki Finland.

Ni mashindano ya pili kwa ukubwa baada ya Olimpiki ambapo nchi 204 zinashiriki mashindano hayo mwaka huu. Tangu kuanzishwa kwa mashindano hayo mwaka huu ndiyo mwaka ambao Tanzania imeleta timu kubwa ya wanariadha 8, ambao ina mchanganyiko wa wanaume na wanawake na pia kuna wakimbiaji wa mbio za uwanjani.
Wanariadha wote wanaoshiriki wamefikia viwango vinavyotakiwa na Shirikisho la Riadha Duniani (IAAF)

Health Nusu Marathon Kufanyika Dar Aprili 26

April 21, 2017


Katibu Mkuu wa Taasisi ya Tanzania Health Summit Bi. Rebecca John (katikati) akisisitiza jambo kwa wandishi wa habari (hawapo pichani) wakati akielezea maandalizi ya mbio za heart marathon na upimaji wa afya yenye lengo la kuisaidia serikali kupunguza magonjwa yasiyoambukizika mapema hii leo jijini Dar es Salaam, kushoto ni Katibu Mkuu Msaidizi wa Chama cha Riadha Tanzania Bi. Ombeni Zavara na kulia ni Katibu Mkuu Chama cha Riadha Mkoa wa Dar es Salaam Bw. Lucas Nkungu.
Katibu Mkuu Msaidizi wa Chama cha Riadha Tanzania Bi. Ombeni Zavara akizungumza na wandishi wa habari (hawapo pichani) juu ya ya mbio za heart marathon na upimaji wa afya yenye lengo la kuisaidia serikali kupunguza magonjwa yasiyoambukizika mapema hii leo jijini Dar es Salaam, kulia ni Katibu Mkuu wa Taasisi ya Tanzania Health Summit Bi. Rebecca John.
Mwenyekiti wa Taasisi ya Tanzania Health Summit Dkt. Omary Chillo (kulia) akifafanua jambo kwa wandishi wa habari (hawapo pichani) wakati akielezea maandalizi ya mbio za heart marathon na upimaji wa afya yenye lengo la kuisaidia serikali kupunguza magonjwa yasiyoambukizika mapema hii leo jijini Dar es Salaam, katikati ni Katibu Mkuu Chama cha Riadha Mkoa wa Dar es Salaam Bw. Lucas Nkungu na kushoto ni Katibu Mkuu wa Taasisi ya Tanzania Health Summit Bi. Rebecca John.

……………..

Na Nuru Juma-Maelezo

Taasisi ya Tanzania Health Summit yaandaa mbio za nusu Marathon na Upimaji wa afya kwa lengo la kusaidia juhudi za serikali katika kupunguza magonjwa yasioambukiza, mbio hizo zinazotarajia kufanyika Aprili 26 katika barabara ya Kaole iliyopo Masaki jijini Dar es Salaam.

Hayo yamesemwa leo na Katibu Mkuu wa Taasisi hiyo Rebecca John wakati alipokutana na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam kwa lengo la kuhamasisha jamii kushiriki.

“Kamati ya maandalizi ya ya mbio za Heart Marathon inapenda kuwa taarifu wadau wote wa sekta ya afya hapa nchini na jamii kwa ujumla juu ya mbio za Heart Marathon na upimaji wa afya ili kuungana na serikali katika juhudi za kupunguza magonjwa yasiyoambukiza” alisema Rebecca.

Aliongeza kuwa kwa mwaka huu mbio hizi zitashirikisha washiriki zaidi ya elfu mbili kutoka rika mbalimbali wakiwemo vijana, watoto, wazee, makundi ya watu wenye ulemavu na watu wenye magonjwa yasiyoambukiza.

Pia washiriki watapata nafasi ya kupima afya magonjwa mbalimbali kama vile shinikizo la damu ,wingi wa sukari katika damu, kiasi cha mafuta mwilini, uchunguzi wa uvimbe katika matiti na kupata ushauri wa wataalam kuhusiana na vyakula bora, magonjwa ya moyo na mishipa ya damu.

Aidha Bi. Rebecca aliongeza kuwa washiriki watakimbia umbali tofauti, kwani kuna mbio ndefu za kilometa 21.1 kwa ajili ya wakimbiaji wazoefu, kilometa 10 kwa wakimbiaji wa kati, kilometa 5 kwa wakimbiaji wa kawaida, kifamilia na kampuni na mbio za watoto chini ya miaka 12 ni meta 700 na zawadi itatolewa kwa mshindi wa kilometa 21.1 pekee kwa kiasi cha shilingi laki tano.

Kwa upande wake Rais wa Tanzania Health Summit Dr.Omary Chillo alisema kuwa washiriki watatakiwa kutoa kiasi kidogo cha fedha kwa ajili ya kununua flana pamoja na kifaaa maalum cha kuhesabia muda wakati wa kukimbia ila maji ya kutosha yatatolewa bure kwa ajili ya wakimbiaji.

Aliongeza kuwa wameimarisha ulinzi kwa kushirikiana na jeshi la polisi na ili kulinda usalama kwa washiriki na wananchi watakaokuwepo katika mashindano hayo.

“wananchi wasiwe na wasiwasi wa usalama kwani tutashirikiana na jeshi la polisi ili kuimarisha usalama na tumeweza kupata baraka nyingi kutoka kwao kwa kuweza kushirikiana nao” aliongeza Chillo.

Pia Katibu msaidizi wa Chama cha Riadha nchini Bi Ombeni Zavala alisema anashukuru wananchi wanavyoweza kujitokeza katika mashindano hayo na pia anawaomba wananchi hasa vijana waendelee kujitokeza kwa wingi kwani wanaweza kupata nafasi ya kuunda timu ya Taifa ya vijana chini ya miaka 17.

Naye Sajenti Isaya Mlokozi kutoka kanda ya usalama barabarani alisema jeshi la polisi kikosi cha usalama barabarani litahusika vizuri katika sehem inayowahusu kuhakikisha watu wanafanya zoezi hilo kwa hali ya usalama na litajumuika na wananchi popote pale watakapokuwa wanakwenda.

Mashindano haya mwaka jana yalifanyika katika Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam lakini kutokana na kuongezeka kwa watu mwaka huu yatafanyikia barabara ya kaole yenye kauli mbiu ‘piga hatua moja mbele ya magonjwa sugu’

RT Yataja Majina 23 Waliochaguliwa kuunda timu ya Taifa ya Vijana

April 17, 2017
Na Mwandishi Wetu
RIADHA Tanzania (RT) imetangaza majina 23 kwa ajili ya kuunda timu ya taifa ya vijana wenye umri chini ya miaka 17 kwa ajili ya kushiriki katika mashindano ya Kanda ya Tano ya Afrika yatakayofanyika jijini Dar es Salaam mapema mwezi ujao.
Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa RT, Whilhem Gidabuday, timu hiyo itapiga kambi katika hosteli za Filbert Bayi zilizoko Mkuza Kibaha kuanzia Jumanne chini ya makocha Robert Kalyahe na Mwinga Mwanjala.
Timu hiyo inaundwa na wachezaji 12 wavulana wakatu wasichana katika timu hiyo wako 11 ma watashiriki katika michezo yam bio za meta 100, 200, 400, 800, 1500 na 3000 pamoja na miruko na mitupo.


Gidabuday alisema kuwa kambi hiyo itagharimu kiasi cha sh Milioni 20 kuanzia timu hiyo itakapokuwa kambini kwa karibu siku 20, wakati wa mashindano na huduma zingine.


Mbali na wenyeji Tanzania Bara, nchini zingine zitakazoshiriki ni pamoja na Zanzibar, Uganda, Kenya, Rwanda, Sudan, Sudan Kusini, Ethiopia, Eritrea na Djibout.


Timu hiyo ilichaguliwa jana mara baada ya kumalizika kwa mashindano ya wazi ya taifa yaliyofanyika kwenye Uwanja wa Taifa na kuhudhuriwa na mikoa michache.
Baadhi ya wanariadha walioshiriki walitoka katika mikoa ya Dar es Salaam, Morogoro, Arusha na Manyara, ambapo shule ya Filbert Bayi iliyopo mkoani Pwani, imeto wachezaji watano katika timu ya wasichana kutokana na umahiri wao.

Ukiondoa baadhi ya kasoro zilizokuwepo ikiwemo kutokuwa na huduma ya kwanza wala gari la wagonjwa, wachezaji wakishiriki bila ya kuwa na namba za kuwatambua na kuleta ugumu kwa waandishi wa habari kujua nani ni nani, mashindano yalienda vizuri.






















Mwanariadha wa Kimataifa, Alphonce Simbu Kuanza Safari ya Kushiriki London Marathon

April 17, 2017



Na Mwandishi Wetu

MWANARIADHA wa kimataifa wa Tanzania, Alphonce Simbu kesho Jumatatu atapanda pipa kwenda Afrika Kusini akiwa njiani kwenda Uingereza, ambako atashiriki London Marathon Jumapili ijayo Aprili 23.

Simbu anapitia Afrika Kusini kwa ajili ya kupatiwa viza ya dharura ya kuingia Uingereza baada ya kuikosa ile ya kawaida jijini Dar es Salaam.

Katibu Mkuu wa Riadha Tanzania (RT), Wilhelm Gidabuday alisema jana kuwa, Simbu ataondoka kesho Jumatatu kwenda Afrika kusini kushughulikia viza ya kuingia Uingereza kabla ya kwenda nchini humo ambako Jumapili atashiriki London Marathon.

Simbu alifuzu kwa mbio hizo baada ya kumaliza katika nafasi ya tano katika Michezo ya Olimpiki iliyofanyika Rio de Janeiro, Brazil 2016 kabla ya kushinda mbio za Mumbai Marathon.

Kwa mujibu wa Gida, tayari mwanariadha huyo ameingia katika orodha ya wanariadha bora kabisa duniani na ndio maana waandaaji wa London Marathon kuna fedha atapewa mara tu atakapoanza mbio hizo (Appearance Fees).

Gidabuday alisema kuwa Simbu hata kama hatashinda mbio hizo lakini akimaliza tu amejihakikishia fungu nono na kama akimaliza, basi ataondoka na maelfu ya dola za Marekani.

Simbu endapo atashinda mbio hizo za London Marathon ataondoka na kitita cha dola za Marekani 55,000 kama zaidi yash Milioni 150, na kama atafanikiwa kuvunja rekodi ataongezewa dola za Marekani 25,000 (ikiwa ni zaidi ya sh Mil 50),

Mshindi wa kwanza hadi wa 12 wa mbio hizo ataondoka na kitita cha fedha, huku wale watakaokimbia muda bora bbila kujali kama umevunja rekodi ya njia au ya dunia, nao wataongezewa fedha za bonasi.

Athletics Body to Move Its Haedquarters to Dodoma

December 22, 2016
Left, Secretary General (AT) Wilhelm Gidabuday and the Former New York City Marathon Champion, Juma Ikangaa. Picture by Gadiola Emanuel.



By Zephania Ubwani

Arusha — Athletics Tanzania (AT) may be the first national sports association to shift its head offices from Dar es Salaam to the designated capital Dodoma, according to its recently elected secretary general, Wilhelm Gidabuday.

The body is already in contact with the Capital Development Authority (CDA), a government institution in charge of infrastructure development in Dodoma, to secure a plot for construction of its headquarters. "We need a plot for our permanent home. After securing it, we will apply for a grant to meet the cost of construction," he told The Citizen here on Monday during an interview on a wide range of issues

He said AT president Anthony Mtaka, who doubles as the Simiyu regional commissioner, has been in touch with CDA officials over the issue.

"After getting the plot, we will seek a title deed we will use as collateral to secure a loan for the project," he said, noting that they will approach the social security institutions for financial support.

Gidabuday, a former national athlete and until recently, a coordinator of various athletics promotion programmes, was elected the new AT secretary general early this month.

He succeeded Suleiman Nyambui who is now an athletics coach in Brunei, a South East Asia sultanate.

He said he would address the major challenges facing the association, including lack of office accommodation that merits its status, working equipment and competent staff for its secretariat.

"We need a modern, spacious and well equipped office which will suffice all our administrative needs," he said, noting that AT, which is one of the oldest sports associations in the country, currently does not have an office that meets its requirements.

"Presently, I can dare say, we have no clear office. There is a room near the Uhuru Stadium, but it's in poor shape," he said, adding that he would fight for a comfortable office space in Dar es Salaam before the Dodoma project is realised.

The long-term plan is to construct the multi-purpose building in Dodoma which will be known as Riadha Tanzania House. Besides serving as the permanent home for AT, some rooms would be rented out to other institutions.

However, Gidabuday insisted that their dreams for a permanent home would depend on support from the government, especially the ministry responsible for sports, CDA, the National Sports Council (NSC) as well as the International Association of Athletics Federation (IAAF), a governing body for the athletics in the world headquartered in Monaco.

TANAPA yaiongezea nguvu timu ya RT, kwa ajili ya wanariadha wanaojiandaa na Olimpiki

July 26, 2016

Meneja Mawasiliano wa Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA) Pascal Shelutete akitoa neno la ukaribisho kwa wanahabari na wageni wengine katika hafla fupi ya kukabidhi hundi kwa wanariadha wanaounda timu ya taifa, inayojiandaa na mashindano ya Olimpiki yatakayoafanyika mwezi Agosti  nchini Brazil.
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA) Allan Kijazi,akizungumza wakati wa hafla fupi ya kukabidhi hundi ya Shilingi Milioni tano kwa wanariadha wanaounda timu ya taifa inayojiandaa na mashindano ya Olimpiki.
Mkurugenzi Mkuu  wa Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA) Allan Kijazi akikabidhi mfano wa hundi ya Shilingi Milioni tano kwa Rais wa Shirikisho la Riadha Tanzania (RT) Anthony Mtaka kwa ajili ya kusaidia wanariadha wanaounda timu ya taifa wakijiandaa na mashindano ya Olimpiki. 
Mkurugenzi Mkuu  wa Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA) Allan Kijazi akikabidhi "Track Suit "maalumu zenye maandishi na nembo yanayotangaza vivutio vya utalii vilivyopo nchini kwa Rais wa Shirikisho la Riadha Tanzania (RT) Anthony Mtaka kwa ajili ya kusaidia wanariadha wanaounda timu ya taifa wanaojiandaa na mashindano ya Olimpiki
Rais wa Shirikisho la Riadha Tanzania (RT) Anthony Mtaka akizungumza mara baada ya kukabidhiwa hundi pamoja na mavazi maalumu kwa ajili ya wanariadha hao .
Baadhi ya viongozi wa Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA) waliohudhuria hafla hiyo.kutoka kushoto Mkurugenzi wa Utalii na Masoko,Ibtahim Musa,Meneja Utalii Johnson Manase na Mhifadhi Vitalis Uruka.
Wanariadha watakaoiwakilisha nchi katika mashindano ya Olimpiki katika jiji la Reo De Jeneiro nchini Brazil wakiwa katika mavazi maalumu yanaotangaza vivutio vilivyoko nchini.
Mkufunzi wa Wanariadha wanaojiandaa na mashindano ya Olyimpiki ,Francis John akizungumzia matarajio yake juu ya vijana hao.
Mmoja wa Wanariadha hao,Alphonce Felix Simbu akizungumza mara baada ya kupoke msaada kutoka  TANAPA.
Baadhi ya Wanahabari na wageni wengine waliofika katika ofisi za Makao Makuu ya Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA) kushuhudia makabidhiano hayo.
Mwanariadha Said Makuka atakayepeperusha bendera ya Tanzania katika michuano ya Olyimpiki nchini Brazil.
Mwanariadha Sara Ramadhan ,mwanadada pekee atakayepeperusha bendera ya Tanzania katika michuano ya Olyimpiki nchini Brazil.
Mwanariadha Alphonce Felix atakayepeperusha bendera ya Tanzania katika michuano ya Olyimpiki nchini Brazil.
Mwanariadha Fabian Joseph atakayepeperusha bendera ya Tanzania katika michuano ya Olyimpiki nchini Brazil.
Wanariadha wanne watakao iwakilisha Tanzania katika Michuano ya Olyimpiki nchini Brazil wakiwa katika picha ya pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA) Allan Kijazi pamoja na Rais wa Shirikisho la Riadha Tanzania (RT) Antony Mtaka ,wengine kutoka kulia ni Mkufunzi wa wanariadha hao,Francis John na anyefuatia ni Mkurugenzi wa Utalii na Masokowa Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA) Ibrahim Musa.

Na Dixon Busagaga wa Michuzi Blog,Kanda ya Kaskazini.

SHIRIKA la Hifadhi za Taifa (TANAPA) limetangaza  kutumia fursa ya mashindano ya Olyimpiki yanayotarajia kuanza mwezi ujao katika jiji la Rio de Janeiro nchini Brazili kutangaza vivutio vya utalii kupitia wanariadha wa Tanzania.

Hadi sasa ni wanariadha wanne ,wakiume watatu na wa kike mmoja ndio waliofuzu kushiriki mashindano hayo na tayari wako kambini katika hosteli za Chuo cha Misitu cha FITI zilizoko West Kilimanjaro wilayani Siha.

Akiongea mjini Arusha wakati akikabidhi msaada wa fedha na vifaa kwa ajili ya wanariadha hao Mkurugenzi Mkuu wa TANAPA,Allan Kijazi amesema wameamua kutumia fursa hiyo pia kusaidia wanariadha hao wanaoiwakilisha nchi katika mashindano hayo ili waweze kurejea na medali.

Akishukuru kwa msaada huo Rais wa Shirikisho la Riadha nchini ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa wa Simiyu AnthonY Mtaka amesema fedha hizo zitatumika kwa ajili ya kuwakatia bima ya Afya mwaka mmoja wanariadha hao pamoja na familia zao ili wanapokua nchini Brazili wasiwe na mawazo mengi kuhusiana na familia zao walizoziacha hapa nchini.

Naye mmoja wa wanariadha waliofuzu kushiriki mashindano hayo Alphonce Felix pamoja na mkufunzi wa timu hiyo ya Riadha Francis John wameushukuru uongozi wa Riadha kwa kuiwezesha timu hiyo kukaa kambini kwa miezi saba na kuahidi safari hii timu hiyo haiendi kushiriki bali kupambania medali.

Wanariadha waliopo katika timu hiyo ya taifa wanaotarajiwa kwenda Brazili ni mwanamke pekee Sara Ramadhani, Fabiani Joseph, Saidi Makuka na Alfonce Felix .

Usajili Azania Kids Run 2016 wapamba moto

June 02, 2016


MCHAKATO wa usajili wa washiriki wa Mbio za Watoto za Azania Bank Kids Run 2016, umezidi kushika kasi, huku siku tatu zikiwa zimesalia kabla ya kufanyika kwake Juni 5 kwenye Viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam.

Akizungumza jijini Dar es Salaam, mmoja wa waratibu wa mbio hizo, Wilhelm Gidabuday, alisema kufikia jana mchana, mchakato wa usajili ulikuwa ukiendelea vema, ambako wazazi na walezi wamejitokeza kusajili watoto wao.

Gidabuday alisema kuwa, matarajio ni kusajili watoto wapatao 2,000 walio na umri chini ya miaka 16, ambao watashiriki Azania Bank Kids Run 2016, mbio zilizogawanywa katika kategori tano za kilomoita 5, km 2, km 1, mita 100 na mita 50.
Alibainisha kuwa, fomu za ushiriki zinapatikana katika Matawi ya Azania Bank popote jijini Dar es Salaam, pamoja na Ofisi za Shirikisho la Riadha Tanzania (RT), pamoja na Ofisi za BMT zilizoko Samora Avenue katikati ya jiji. Aliwataka wazazi na walezi ambao hawajachukua fomu za ushiriki wa watoto wao, kuchangamkia mchakato huo kwa kufika katika vituo husika na kununua fomu hizo kwa shilingi 2,000 tu, ili kuwawezesha watoto kushiriki na kushinda zawadi.

Naye, Ofisa Masoko Mwandamizi wa Azania Bank inayodhamini mashindano hayo, Othman Jibrea, alisisitiza umuhimu wa wazazi na walezi kusajili watoto wao katika Azania Bank Kids Run, ili kufikia lengo lao la kuibua vipaji vipya vya riadha.

Jibrea alibainsiha kuwa, Azania Bank imejitosa kudhamini mbio hizo kutokana na mlengo wake wa kuibua vipaji vichanga katika riadha, hivyo ili kufikia lengo, wazazui na walezi hawana budi kujitokeza kwa wingi kusajili watoto wao.

Alizitaja zawadi za mbio za Kilomita tano kuwa ni Sh. 200,000 kwa mshindi wa kwanza, Sh. 150,000 kwa mshindi wa pili na Sh. 100,000 kwa mshindi wa tatu, wote wakitarajiwa pia kupata medali, begi lenye vifaa vya shule na sare za michezo (track suit).

Jibrea alibainisha kuwa, mshindi wa kwanza wa mbio za kilomita 2 atajinyakulia Sh. 100,000, mshindi wa pili Sh. 75,000 na mshindi wa tatu Sh. 50,000, pamoja na medali, begi lenye vifaa vya shule na sare za michezo.

Katika mbio za kilomita 1, Jibrea alitaja zawadi za washindi kuwa ni Sh. 75,000 kwa mshindi wa kwanza, 50,000 kwa mshindi wa pili na Sh. 40,000 kwa wa tatu, ambao watapata zawadi ya ziada ya medali, begi lenye vifaa vya shule na sare za michezo.

"Pia, washindi wa nne hadi wa 10 wa mbio hizo, watapata kifuta jasho cha Sh. 15,000, begi lenye vifaa vya shule na sare za michezo. Nia ni kuwafanya watoto watakaoshiriki kutotoka bure mwishoni mwa mashindano," alisema Jibrea.
 

Copyright © 2015 - 2025 Athletics Tanzania All Right Reserved

Developed by Gadiola Emanuel
Theme By AP | Developed By Gadiola Emanuel