Showing posts with label Kitaifa. Show all posts
Showing posts with label Kitaifa. Show all posts

Washindi NBC Dodoma Marathon Kuiwakilisha Tanzania Kimataifa, Dkt Ndumbaro Athibitisha Ushiriki Wake Mbio Za Km 42

July 23, 2024

Serikali imesisitiz dhamira yake ya kutumia mbio za NBC Dodoma Marathon kama chanzo cha kuwapata wanariadha sahihi watakaoliwakilisha taifa kwenye mashindano ya kimataifa yakiwemo mashindano ya Olympic na Mashindano ya Jumuiya ya Madola (Commonwealth).  Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt Damas Ndumbaro amebainisha dhamira hiyo ya serikali jijini Dar es Salaam leo huku akithibitisha nia yake ya kukimbia km 42 (full marathon) kwenye mbio hizo zinatotarajiwa kufanyika jijini Dodoma, Julai 28 mwaka huu. 

Lengo kuu la mbio hizo zinazotarajiwa kuongozwa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ni kukusanya fedha ili kusaidia mapambano dhidi ya saratani ya shingo ya kizazi na  kutoa ufadhili wa elimu kwa wakunga  ili kuboresha afya ya mama wa mtoto.

Akizungumza kwenye mkutano na waandishi wa habari Makao Makuu ya benki ya NBC  akiwa sambamba na mwenyeji wake Mkurugenzi Mtendaji wa benki hiyo, Bw Theobald Sabi,  Dkt Ndumbaro pamoja na kusifia jitihada za benki hiyo katika kuinua sekta ya michezo nchini, alisema kwasasa taifa linakabiliwa na uhaba mkubwa wa wanariadha wenye sifa ya kushiriki mashindano ya kimataifa hivyo serikali imejipanga kutumia mbio hizo kutambua wanariadha wenye sifa sahihi kwa ajili ya maandalizi ya mashindano mbalimbali ya kimataifa.

“Kwasasa kwenye mashindano ya Olympic tunakwenda na wanariadha wachache sana kwasababu hatuna maandalizi ya kutosha. Hivyo NBC Dodoma Marathon ni moja ya chanzo cha kupata wanariadha wazuri ili baada ya mbio hizi tuweze kuwatamuba na kuwapa mafunzo zaidi ili mashindano ya ‘Commonwealth’ na Olympic na mengine mbalimbali ya kimataifa tuwe na wanariadha wengi zaidi.’’ Alibainisha Dkt. Ndumbaro huku akipongeza maandalizi ya mbio yenye kuzingatia viwango vya kimataifa.

Aidha Dkt. Ndumbaro aliipongeza benki hiyo kwa jitihada mbalimbali za kuendeleza sekta ya utamaduni, sana ana michezo kupitia mikakati mbalimbali ikiwemo udhamini wa michezo na huduma za kibenki zinazolenga kuwasaidia wadau mbalimbali wa sekta hizo.

Tofauti na mbio hizi, jitihada za benki ya NBC kwenye kuinua sekta ya michezo zinaonekana kupitia udhamini wake kwenye ligi za NBC Premier League, NBC Championship na NBC Youth league ambapo imewekeza kiasi cha Sh.32.6 Bilioni kwenye ligi hizo. Pia benki hii ina inashiriki katika uwezeshaji kiuchumi kwa wasanii kupitia mfuko wa maendeleo ya sanaa nchini sambamba na kusimamia kamati ya Hamasa ya Timu za Taifa ambapo mpaka sasa imeshakusanya kiasi cha Shilingi 2 bilioni kati kutokana na ahadi za awali za Sh.4 bilioni zilizopokelewa katika hafla ya uzinduzi wa kamati hiyo,’’ alisema.

Awali akizungumza kwenye mkutano huo, Sabi alisema jitihada za benki hiyo katika kuendeleza sekta ya michezo nchini kwa kiasi kikubwa inachagizwa na imani ya benki hiyo kuwa sanaa na michezo ni nguzo ya ajira na kuunganisha taifa.

“Kwa mfano kupitia udhamini wetu kwenye ligi tatu muhimu za mpira wa miguu hapa nchini, mbali na kuzalisha vipaji tumezalisha ajira za moja kwa moja zaidi ya 7,000 na mamilioni ya ajira zingine kwenye mnyororo wa uchumi. Zaidi pia kupitia mbio hizi za NBC Dodoma Marathon kwa kushirikiana na wadau wetu mbalimbali tunalenga kukusanya fedha kusaidia juhudi za Serikali katika kuboresha ya afya ya mama na mtoto kupitia mapambano dhidi ya saratani ya shingo ya kizazi kwa wanawake na kutoa ufadhili kwa wakunga,’’ alisema.

Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt Damas Ndumbaro (kushoto) akipokea sweta maalum la mbio za NBC Dodoma Marathon kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC, Theobald Sabi ikiwa ni ishara ya kumkaribisha rasmi Waziri huyo kwenye mbio hizo zinazotarajiwa kufanyika Julai 28 mwaka huu kwenye Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma zikiwa na lengo la  kukusanya fedha ili kusaidia mapambano dhidi ya saratani ya shingo ya kizazi na  kutoa ufadhili wa elimu kwa wakunga  ili kuboresha afya ya mama wa mtoto Makabiziano hayo yamefanyika  makao makuu ya benki hiyo jijini Dar es Salaam leo.


Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC, Theobald Sabi (kulia) akimpongeza Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt Damas Ndumbaro (kushoto) baada ya kuthibitisha dahamira yake ya kukimbia km 42 kwenye mbio za NBC Dodoma Marathon zinazoratibiwa na benki hiyo kwa lengo la  kukusanya fedha ili kusaidia mapambano dhidi ya saratani ya shingo ya kizazi na  kutoa ufadhili wa elimu kwa wakunga  ili kuboresha afya ya mama wa mtoto. Dkt Ndumbaro  amethibitisha dhamira hiyo leo jijini Dar es Salaam.


Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt Damas Ndumbaro (kushoto) akimpongeza Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya mbio za NBC Dodoma Marathon Bi Tatiana Masimba kwa maandalizi mazuri yam bio hizo zinazotarajiwa kufanyika Julai 28 mwaka huu kwenye Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma zikiwa na lengo la  kukusanya fedha ili kusaidia mapambano dhidi ya saratani ya shingo ya kizazi na  kutoa ufadhili wa elimu kwa wakunga  ili kuboresha afya ya mama wa mtoto


Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt Damas Ndumbaro (kushoto) akizungumza na waandishi wa Habari (hawapo pichani) kuhusu mbio za NBC Dodoma Marathon pamoja mchango wa benki ya NBC katika kuendeleza sekta ya michezo nchini.   Kulia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC, Theobald Sabi



Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC, Theobald Sabi (kulia) akizungumza na waandishi wa Habari (hawapo pichani) kuhusu mbio za NBC Dodoma Marathon pamoja mchango wa benki ya NBC katika kuendeleza sekta ya michezo nchini. Kushoto ni Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt Damas Ndumbaro.

SASA RIADHA NA WAANDAAJI " RACE ORGANIZERS" DAM DAM

March 05, 2023

 

Kutoka Kulia: Ofisa wa BMT Charles Maguzu, Makamu wa Rais William Kallaghe na Mjumbe wa Kanda ya Kaskazini Alfredo Shahanga.


NA TULLO CHAMBO, RT

BAADA ya kutokea sintofahamu ya muda mrefu kati ya Shirikisho la Riadha Tanzania (RT), na waandaaji wa matukio mbalimbali ya mbio za barabarani (RO's), hatimaye imefikia tamati.

Tamati hiyo imefikiwa baada ya kikao cha pamoja kati ya RT, RO's na Baraza la Michezo la Taifa (BMT), kilichofanyika jijini Dar es Salaam, Machi 4 mwaka huu.
Katika kikao hicho kilichokuwa chini ya Makamu wa Rais wa RT , William Kallaghe na Ofisa Michezo BMT, Charles Maguzu, kilijadili kwa kina changamoto zinazokabili pande zote tatu.
Baada ya majadiliano ya takribani saa sitaa, pande zote zilipitia vifungu mbalimbali vya kikanuni na kuafikiana kuziheshimu ili kujenga ustawi bora wa mchezo wa riadha nchini.

Kikubwa kilichokaziwa, ni waandaaji kuheshimu mamlaka zilizopo na mamlaka kutenda haki kwa wateja wao (RO's).
Kikubwa Makamu wa Rais wa RT, Kallaghe aliwataka waandaaji kuheshimu na kushirikiana vyema na vyama vya riadha vya mikoa, na kwamba kuanzia hivi sasa waandaaji wanatakiwa kupata baraka za vyama vya mikoa kabla ya kuanza kutangaza matukio yao.

RT YATEKELEZA MAAGIZO YA BMT

March 05, 2023

 

Kulia ni Makamu wa Rais wa Shirikisho la Riadha Tanzania RT , Ndugu William Kallaghe akikabidhi ripoti kwa Katibu Mkuu Mtendaji wa BMT, Bi. Neema Msitha Jijini Dar es Salaam.


SHIRIKISHO la Riadha Tanzania (RT), Machi 3, 2022, limetekeleza agizo la Baraza la Michezo la Taifa (BMT), baada ya kukabidhi ripoti ya mapato na matumizi.

Ripoti hiyo imekabidhiwa na Makamu wa Rais wa RT, William Kallaghe, kwa Katibu Mtendaji wa BMT, Neema Msitha.
BMT ilifanya kikao na Kamati ya Utendaji ya RT,    Januari 21 kwenye moja ya kumbi za Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam, na moja ya maelekezo ya Baraza, ilikuwa ni kuitaka RT kuwasilisha ripoti ya mapato na matumizi 2020/21 hadi 2021/22.

Baada ya kuipokea ripoti hiyo, Katibu Mtendaji BMT, Msitha, alisema watakaa na kuifanyia kazi.

RT YAWATAKA WATAALAM WA RIADHA NCHINI KUWASILISHA TAARIFA ZAO

February 05, 2023

 





NA TULLO CHAMBO, RT

SHIRIKISHO la Riadha Tanzania (RT), limewataka wataalamu wote wa mchezo huo kuwasilisha taarifa zinazoonyesha fani zao.
Agizo hilo, limetolewa na Kaimu Katibu Mkuu RT, Wakili Jackson Ndaweka, ambako amewataka makatibu wa vyama vya riadha mikoa yote ya Tanzania Bara, kuwajulisha wataalam wa riadha waliopo mikoani mwao, kuwasilisha taarifa zinazoonyesha fani zao katika mchezo huo. 

Wakili Ndaweka,amesema RT inakusudia kuendesha kozi mbalimbali za kuboresha uwezo wa wataalamu wa mchezo wa riadha waliopo na kuzalisha wengine katika fani ambazo zina upungufu. 

"Ili mpango huu uweze kutekelezeka kwa ufanisi, ni lazima kuwa na taarifa za wataalamu wa Riadha nchini, zitakazowezesha kuainisha maeneo yenye upungufu na kuyawekea mpango maalum," alisema na kufafanua. 

Taarifa zinazotakiwa zinapaswa kuwasilishwa kupitia wasifu 'CV', ambayo inapaswa kuambatanishwa na vivuli vya vyeti vya elimu ya Riadha na elimu ya kawaida. 

Wakili Ndaweka, alisema takwimu hizo ni muhimu sana kwa maendeleo ya mchezo wa riadha nchini. 

"Makatibu wanapaswa kuwajulisha wataalam waliopo kwenye mikoa yao, wawasilishe taarifa hizo kupitia anuani ya barua pepe ya shirikisho ambayo ni tan@mf.worldathletics.org si zaidi ya tarehe 20/02/2023," alisisitiza Ndaweka.

RT YAANIKA MATUKIO MANNE MAKUBWA YA KIMATAIFA 2023

February 04, 2023

 


| Yataka ushirikiano, uwajibikaji ngazi zote

|Timu ya Cross Country kuagwa Februari 14

NA TULLO CHAMBO, RT

SHIRIKISHO la Riadha Tanzania (RT), limeanika matukio manne makubwa ya kimataifa yanayolikabili mwaka 2023 na kusisitiza uwajibikaji wa pamoja kwa ngazi zote ili kuleta matokeo chanya.

Akizungumza na Wanahabari jijini Mwanza Februari 3, Rais wa RT, Silas Lucas Isangi, ameyataja matukio hayo ni Mashindano ya Mbio za Nyika 'Cross Country' ya Dunia, Bathurst, Australia Februari 18, Mashindano ya Vijana Afrika Mashariki (EAAR), U 18 na 20 Tanzania itakuwa mwenyeji Machi 10-11.

Tukio la tatu, Isangi alitaja ni Mashindano ya Afrika U 18 na 20 Lusaka Zambia  Aprili 27 hadi Mei 3.

"Pia kuna mashindano ya Common Wealth U 18 huko Trinidad na Tobago Agosti 4-11, vile vile All Africa Games Julai 4-23 nchini Ghana na Mashindano ya Dunia Budapest, Hungary" alisema na kuongeza.

Kwa kifupi mwaka huu uko bize sana, hivyo viongozi wa Riadha ngazi za chini kabisa, lazima wote tuamke na kutimiza wajibu kwa vitendo.

Rais Isangi, aliitaka mikoa yote ifanye mashindano ya vijana ili kufanikisha upatikanaji wa timu ya Taifa U 18 na 20 yenye tija. Pia ushiriki wao kwenye mashindano ya Taifa uwe wenye tija.

TIMU YA TAIFA CROSS COUNTRY
Rais Isangi, amesema timu hiyo imeanza kambi toka Februari Mosi katika Hoteli ya Mvono, Ngaramtoni jijini Arusha kwa gharama za shirikisho asilimia 100.

Amesema, timu itakaa kambini hadi Februari 12, itakapokwenda jijini Dar es Salaam tayari kwa kuagwa Februari 14, kabla ya kukwea pipa kwa safari ya Australia.

Amesema timu hiyo itakuwa chini ya Kiongozi wa msafara, Wakili Jackson Ndaweka ambaye ni Kaimu Katibu Mkuu RT, Kocha Denis Male, huku wachezaji ni Mathayo Sombi, Inyasi Sulle, Fabian Nelson na Josephat Gisemo.

"Maandalizi yote yamekamilika ikiwamo tiketi, visa na vibali vyote vya serikali vimekamilika," alisema na kuishukuru serikali kupitia Baraza la Michezo la Taifa (BMT), kwa kusaidia katika maandalizi hayo.

MIKOA YATAKIWA KUHAKIKISHA MASHINDANO YA RIADHA VIJANA YANAANZIA NGAZI YA WILAYA

January 27, 2023

 


Kaimu Katibu Mkuu RT, Wakili Jackson Ndaweka.

SHIRIKISHO la Riadha Tanzania (RT), limeitaka mikoa yote nchini kuhakikisha inaendesha mashindani ya Vijana chini miaka 20 na 18 'U-20 U-18' kuanzia ngazi ya Wilaya.


Maelekezo hayo yametolewa na Kaimu Katibu Mkuu RT, Wakili Msomi Jackson Ndaweka, katika barua yake ya Januari 25 kwenda kwa viongozi wa vyama vya mikoa Tanzania Bara.


Amewaelekeza viongozi hao, kukumbuka kwamba kuna jukumu kubwa mbele yao, kwani mwaka huu una mashindano mengi ya vijana wa umri huo.


 Wakili Ndaweka, aliyataja mashindano hayo kuwa ni Afrika Mashariki U-18 na 20, Tanzania ikiwa mwenyeji, ambapo awali yalikuwa yamepangwa kufanyika Kigali, Rwanda.


Alisema, mashindano hayo yatafuatiwa na ya Afrika kwa umri huo Lusaka, Zambia Aprili 27 hadi Mei 3, 2023.


"Ili kuhakikisha nchi inashiriki kwa mafanikio mashindano hayo, lazima mashindano yaanzie ngazi ya Wilaya, kisha Mkoa na mwisho mashindano ya Taifa ya Wazi kwa vijana wa umri huo ambayo yanatarajiwa kufanyika Februari 25," alisema na kuongeza.


 Mashindano ya Wilaya yafanyike kati ya Februari 9-11 na Mikoa Februari 13-19.

 

"Utaratibu huu, unakusudia kuhakikisha wanapatikana wachezaji wenye uwezo mkubwa, ili kuleta tija katika ushiriki wa nchi kwenye mashindano ya kimataifa," alisema Wakili Ndaweka. 


Sambamba na hilo, RT inakusudia na imejipanga kuhakikisha kuwa kalenda yake inafuatwa na matukio yote yanafanyika kama yalivyopangwa.

LADIES FIRST 2023 YAZIDI KUFUNGUA NEEMA RIADHA TANZANIA.

January 26, 2023


Sudan Kusini yaipa shavu RT, Simbu Balozi mpya JICA


NA TULLO CHAMBO, RT


MASHINDANO Maalum ya Riadha ya Wanawake nchini Tanzania maarufu kama Ladies First, yamezidi kufungua ushirikiano wa mchezo huo kimataifa.


Ladies First ikiwa ni wazo la Nguli wa Riadha nchini Tanzania, Kanali mstaafu Juma Ikangaa, imefanyika mwaka huu ukiwa ni msimu wa nne na kushirikisha mikoa 30 Kati ya 31 Tanzania Bara na Visiwani.


Mwaka huu, mashindano hayo yalifanyika January 21 na 22 kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam na kushirikisha zaidi ya wanariadha 186.


Kanali Mstaafu Ikangaa, ambaye enzi zake aliiwakilisha vema Tanzania kimataifa katika mbio za marathoni, ikiwemo nchini Japan, nchi hiyo imekuwa ikimuenzi na kumpa heshima kubwa ambapo hivi sasa ni Balozi wa Hiari wa Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Japan (JICA).


Katika kumuenzi Kanali Ikangaa, Japan ilimtaka kusema kitu ambacho nchi hiyo iifanyie Tanzania, ndipo kwa kushirikiana na wadau wake mbalimbali, akaja na wazo la kuwaenzi na kuhamasisha wanawake kushiriki katika mchezo wa Riadha, hasa ikizingatiwa medali ya kwanza ya kimataifa Tanzania ililetwa na Mwanamke Theresia Dismas mwaka 1964, katika michezo ya All Africa nchini Congo Brazzaville, kupitia mchezo wa Kurusha Mkuki 'Javelin'.


Wazo hilo lilianza kutekelezeka mwaka 2017 kwa mashindano yaliyofanyika Uwanja wa Taifa, sasa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam, ambapo baadhi ya washindi wamekuwa wakipata nafasi ya kwenda kushiriki mbio za Nagai City nchini Japan.

Katibu Mtendaji wa Baraza la Michezo la Taifa Tanzania (BMT), Bi. Neema Msitha, aliipongeza JICA na kampuni mbalimbali za Kijapan zinazofanya kazi nchini, Kanali Ikangaa,serikali ya Tanzania na Shirikisho la Riadha Tanzania (RT), kwa kufanikisha mashindano hayo kwa msimu wa nne sasa.


Bi. Msitha, anasema mashindano hayo yalianza mwaka 2017 na kufanyika kwa mafanikio makubwa miaka mitatu mfululizo hadi 2019 kabla kusitishwa kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo janga la UVIKO 19 'Covid 19'.


"Lengo la mashindano haya ni kuhamasisha ushiriki wa watoto wa kike katika michezo hususan Riadha, kutoa fursa kwa wanariadha wa kike kuonyesha vipaji vyao na kuendeleza vipaji vya wanariadha ambao wataiwakilisha nchi katika mashindano ya kitaifa na kimataifa," anasema Bi. Msitha.


Tangu kuanza kwa mashindano hayo mwaka 2017, Wanariadha wa Tanzania na viongozi wao, wamekuwa wakipata nafasi ya kwenda kushiriki Nagai Marathon, ambapo wanariadha akiwemo Angel John Joseph Yumba, Fabian Nelson Sulle, Fabian Joseph, Alphonce Felix Simbu na wengineo wameweza kung'ara.


Mbali na hilo, Ladies First iliweza kuishirikisha nchi ya Sudan Kusini na kushiriki mashindano ya mwaka 2019 jijini Dar es Salaam.


Mwaka huu 2023, Ladies First imezidi kufungua milango katika mchezo wa Riadha Tanzania, ambapo Sudan Kusini iliwakilishwa na viongozi wake mbalimbali akiwemo Katibu Mkuu wa Wizara ya Michezo nchini humo, Peter Baptist, Balozi wa nchi hiyo nchini Tanzania, Deng Abel na wengineo.

Baptist katika salamu zake, mbali na kushukuru na kupongeza Tanzania kwa mashindano hayo, anasema na kwao wana mashindano kama hayo yajulikanayo kama 'Umoja na Amani', yakilenga kutumia michezo kuhamasisha amani na umoja katika Taifa hilo ambalo liliandamwa na vita miongoni mwao kwa miaka kadhaa.


Mwakilishi huyo, anasema katika kuendeleza ushirikiano na Tanzania, wanatoa mwaliko kwa wanariadha wanne waliofanya vizuri katika Ladies First 2023 wa mbio tofauti ukiondoa mita 5000 kwenda Sudan Kusini kushiriki mashindano hayo yanayotarajiwa kufanyika miezi miwili ijayo.


Mbali na fursa hizo zilizojitokeza Ladies First 2023, nyingine ni kwa Mwanariadha anayefanya vema hivi sasa, Mshindi wa Medali ya Fedha Common Wealth Games 2022, Alphonce Simbu, naye kuteuliwa kuwa Balozi wa Hiari JICA, akiungana na Kanali mstaafu Ikangaa.


Haya ni kati ya mafanikio ya Ladies First 2023, na hakika uwajibikaji ukizidi kuongezeka, bila shaka milango zaidi itazidi kufunguka katika medani ya riadha Tanzania.

 

Copyright © 2015 - 2025 Athletics Tanzania All Right Reserved

Developed by Gadiola Emanuel
Theme By AP | Developed By Gadiola Emanuel