GEAY 'AKICHAFUA' MBEYA TULIA MARATHON 2023

May 06, 2023


 

BINGWA wa Taifa anayeshikilia rekodi ya Marathon Tanzania, Gabriel Gerald Geay amekuwa kivutio kikubwa Mbeya Tulia Marathon, aliposhiriki na kuibuka mshindi katika mbio za mita 1500.

Mbeya Tulia Marathon, imekata utepe Leo Mei 5 kwa mbio za uwanjani, kabla ya kesho Jumamosi Mei 6 kurindima Marathon.

Katika mbio hizo za mita 1500, Geay alianza taratibu raundi ya kwanza akiwa nyuma, kabla ya mzunguko wa pili kupata dhoruba la kuangushwa, lakini alinyanyuka na kukiwasha na hatimaye kuibuka mshindi akitumia dakika 3:58.46.

Geay alifuatiwa na Faraja Damas wa JWTZ aliyetumia dakika 4:00.08 huku nafasi ya tatu ikienda kwa John Joseph pia JWTZ 4:06.25. 

Mashabiki na viongozi mbalimbali waliojitokeza, wakiongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Beno Malisa, walishindwa kujizua kumshangilia Geay wakati akikiwasha katika mbio hizo.

Kwa upande wa wanawake Mita 1500, Magdalena Shauri wa JWTZ, alishinda akitumia dakika 4:31.13 na kufuatiwa na Salma Charles ambaye katoka Zambia na Timu ya Taifa U 18 na 20 iliyoshiriki mashindano ya Afrika, dakika 4:46.55 na wa tatu akiwa ni Mayselina Mbua JWTZ 4:53.16.

Mbali na Geay ambaye katoka kufanya kweli katika mbio kongwe za Boston Marathon nchini Marekani alikoshika nafasi ya pili hivi karibuni, pia mkali mwingine, ambaye pia ni Mshindi wa medali ya Fedha Jumuiya na Mwanamichezo Bora Tuzo za BMT 2022, Alphonce Simbu, naye alikuwepo kushuhudia mbio hizo.

Pia, Timu ya Taifa ya Vijana iliyopumzika hapa ikitokea Ndola Zambia ilikojinyakulia medali mbili katika mashindano ya Afrika, baadhi walipata nafasi ya kushiriki mbio za uwanjani Mbeya Tulia Marathon.

Timu hiyo inatarajiwa kuondoka Mbeya kesho Jumapili kurejea Dar es Salaam.

Pia, mbio hizo zilipambwa program ya watoto 'Kids Athletics', ambayo ilikuwa kivutio kwa watoto wa shule za msingi walioshiriki.

JK AKUTANA NA MWANARIADHA WA KIMATAIFA GABRIEL GERALD GEAY BOSTON, MAREKANI

April 19, 2023

 Jakaya Mrisho Kikwete akiwa na wanariadha Gabriel Geay (kushoto kwake) na Wence Tarimo (kulia kwake) ambao walishiriki katika Mashindano ya Riadha yaliyofanyika Boston, Marekani tarehe 17 Aprili 2023, ambapo Geay aliibuka mshindi wa pili. Kulia ni Mhe. Saada Mkuya, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - Fedha na Uchumi - wa Zanzibar.
Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akipokea zawadi ya jezi toka kwa mhamasishaji mashuhuri Nick Reynolds maarufu kama Bongo Zozo wakati alipoonana na wanariadha Gabriel Geay (kushoto kwake) na Wence Tarimo (kulia kwake) ambao walishiriki katika Mashindano ya Riadha yaliyofanyika Boston, Marekani tarehe 17 Aprili 2023, ambapo Geay aliibuka mshindi wa pili. Kulia ni Mhe. Saada Mkuya, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - Fedha na Uchumi - wa Zanzibar.
Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akiweka saini kwenye kitabu cha mwanariadha Gabriel Geay mjini Boston Marekani, siku moja baada ya shujaa huyo kushika nafasi ya pili kwenye mbio za Boston Marathon.
Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akiwa na wanariadha Gabriel Geay (kushoto kwake) na Wence Tarimo (kulia kwake) ambao walishiriki katika Mashindano ya Riadha yaliyofanyika Boston, Marekani tarehe 17 Aprili 2023, ambapo Geay aliibuka mshindi wa pili. Kulia ni Mhe. Saada Mkuya, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - Fedha na Uchumi - wa Zanzibar na kushoto ni mhamasishaji mashuhuri Nick Reynolds maarufu kama Bongo Zozo.
Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete na Mhe. Saada Mkuya, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - Fedha na Uchumi - wa Zanzibar wakiwa na Watanzania waishio Marekani pamoja na wanariadha Gabriel Geay na Wence Tarimo ambao walishiriki katika Mashindano ya Riadha yaliyofanyika Boston, Marekani tarehe 17 Aprili 2023, ambapo Geay aliibuka mshindi wa pili. Kulia ni mhamasishaji mashuhuri Nick Reynolds maarufu kama Bongo Zozo na kushoto ni mtoto wa Bongo Zozo.
Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akimkabidhi kitabu mwanariadha Gabriel Geay mjini Boston Marekani, siku moja baada ya shujaa huyo kushika nafasi ya pili kwenye mbio za Boston Marathon.

*******

Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete amekutana na Wanariadha Gabriel Geay na Wence Tarimo walioshiriki katika Mashindano ya Marathon yaliyofanyika Boston, Marekani tarehe 17 Aprili 2023.

Gabriel Geay aliibuka mshindi wa pili katika mashindano hayo. Mheshimiwa Rais Mstaafu amempongeza Gabriel Geay kwa ushindi mkubwa na kwa kupeperusha vyema bendera ya Tanzania.

Pamoja na wanariadha hao, walikuwepo pia wahamasishaji mbalimbali akiwemo “Bongo Zozo”. Amewapongeza pia kwa kuhamasisha ushindi huu na kufanikisha kuinua bendera ya Tanzania juu.

Mheshimiwa Rais Mstaafu yuko Boston, Marekani ambapo anashiriki katika kutoa mafunzo kwa Mawaziri wa Fedha kutoka nchi mbalimbali zinazoendelea kupitia Mpango wa Uongozi wa Harvard “Harvard Ministerial Leadership Program”.

Katika mafunzo hayo, Mhe. Saada Mkuya, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - Fedha na Uchumi - wa Zanzibar ameshiriki pia.

RT YAUONGEZEA THAMANI UWANJA WA BENJAMIN MKAPA, DAR

March 12, 2023

 







 NA TULLO CHAMBO, RT


SHIRIKISHO la Riadha Tanzania (RT), kwa ushirikiano na shirikisho la mchezo huo nchini Kenya (AK), wamezindua kifaa maalum cha kupima hali ya hewa kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam.

Kifaa hicho ni maalumu kwa ajili ya kupima ubora wa hali ya hewa sehemu husika, kama iko sawa kwa matumizi ya wanamichezo shiriki wakati wa tukio ama haiko sawa.

Ufungaji wa kifaa hicho ni maagizo ya Shirikisho la Riadha la Kimataifa (WA), ambapo Tanzania imekuwa nchi ya nne barani Afrika kupata teknolojia hiyo. 

Akizungumza  wakati wa uzinduzi huo mbele ya Mgeni rasmi Katibu Mtendaji wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Neema Msitha, Rais wa AK ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Riadha Ukanda wa Afrika Mashariki (EAAR), Luteni Jenerali mstaafu Jackson Tuwei, alisema kifaa hicho ni muhimu kwani binadamu hata wanyama wanahitaji kuishi katika mazingira ya hali ya hewa safi.

Luteni Jenelari Tuwei, alisema teknolojia hiyo imeanza kutumika nchini Kenya, kisha ilifuatiwa na Dakar Senegal, Addis Ababa Ethiopia na Tanzania imekuwa ni nchi ya nne kufungwa katika Uwanja wa Benjamin Mkapa na badae wanatarajia kufunga kifaa hicho nchini Zambia ambako yanatarajiwa kufanyika mashindano ya vijana Afrika Aprili 27 hadi Mei 3.

Kwa upande wake, Katibu wa BMT, Neema Msitha, alishukuru kwa jambo hilo ambalo linauongezea thamani wa Uwanja wa Benjamin Mkapa kimataifa, na kwamba Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan, mbali ya kuipongeza RT kwa kufanikisha jambo hilo lenye manufaa kwa wanamichezo wote watakaokuwa wanautumia uwanja huo, iko tayari kutoa Ushirikiano katika kila  jambo lenye maendeleo kwenye sekta ya michezo na kwamba wadau wote wa michezo wanakaribishwa.

Kifaa hicho kimetengenezwa na taasisi ya mazingira nchini Sweden ijulikanayo kama Stocklohom Environment Instute (SEI).

SASA RIADHA NA WAANDAAJI " RACE ORGANIZERS" DAM DAM

March 05, 2023

 

Kutoka Kulia: Ofisa wa BMT Charles Maguzu, Makamu wa Rais William Kallaghe na Mjumbe wa Kanda ya Kaskazini Alfredo Shahanga.


NA TULLO CHAMBO, RT

BAADA ya kutokea sintofahamu ya muda mrefu kati ya Shirikisho la Riadha Tanzania (RT), na waandaaji wa matukio mbalimbali ya mbio za barabarani (RO's), hatimaye imefikia tamati.

Tamati hiyo imefikiwa baada ya kikao cha pamoja kati ya RT, RO's na Baraza la Michezo la Taifa (BMT), kilichofanyika jijini Dar es Salaam, Machi 4 mwaka huu.
Katika kikao hicho kilichokuwa chini ya Makamu wa Rais wa RT , William Kallaghe na Ofisa Michezo BMT, Charles Maguzu, kilijadili kwa kina changamoto zinazokabili pande zote tatu.
Baada ya majadiliano ya takribani saa sitaa, pande zote zilipitia vifungu mbalimbali vya kikanuni na kuafikiana kuziheshimu ili kujenga ustawi bora wa mchezo wa riadha nchini.

Kikubwa kilichokaziwa, ni waandaaji kuheshimu mamlaka zilizopo na mamlaka kutenda haki kwa wateja wao (RO's).
Kikubwa Makamu wa Rais wa RT, Kallaghe aliwataka waandaaji kuheshimu na kushirikiana vyema na vyama vya riadha vya mikoa, na kwamba kuanzia hivi sasa waandaaji wanatakiwa kupata baraka za vyama vya mikoa kabla ya kuanza kutangaza matukio yao.

19 WAPENYA TIMU YA TAIFA VIJANA EAAR

March 05, 2023


Wanariadha wakichuana kwenye mashindano ya Majaribio Jijini Dar es Salaam.

Makamu wa rais wa shirikisho la Riadha la Tanzania, Ndugu William Kallaghe akizungumza na wanariadha waliopenya kwenye timu ya Taifa ya Vijana ya EAAR Dar es Salaam.


NA TULLO CHAMBO, RT

WANARIADHA 19 wamefanikiwa kuchaguliwa timu ya Taifa ya Vijana chini ya miaka 18 na 20 itakayoiwakilisha Tanzania katika mashindano ya Afrika Mashariki (EAAR U 18 & U 20 yanayotarajiwa kufanyika jijini Dar es Salaam, kuanzia Machi 9 mwaka huu.
Wanariadha hao wamepatikana kupitia mashindano ya wazi ya Taifa, yaliyofanyika Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es  Salaam Machi 4 mwaka huu, ambayo yaliandaliwa na Shirikisho la Riadha Tanzania (RT).

Jopo la Wataalamu wakiongozwa na Makocha wa Taifa wa timu hiyo, Robert Kalyahe na Mwinga Mwanjala, lilichagua wanariadha hao kutokana na viwango ambavyo wanariadha hao walivionyesha na si kutokana na nafasi walizoshika katika mchezo husika.

Aidha makocha hao, walibainisha kuwa wameshuhudia vipaji vipya vingi wameviona na kama vikiendelezwa vitakuja kuwa lulu kwa Taifa siku zijazo.
Kutokana na vijana hao 19 waliofuzu, wengine nane watajumuishwa nao ambao walifanya vema katika mashindano mengineyo ikiwemo Ladies First yaliyofanyika hivi karibuni jijini Dar es Salaam.

Akizungumza mara baada kutangazwa timu hiyo mbele ya viongozi wa mikoa iliyoshiriki Tabora, Mbeya, Pwani, Dar es Salaam, Arusha, Morogoro, makocha mbalimbali na Waandaaji wa Matukio ya Riadha 'Race Organizers' (RO's), Makamu wa Rais wa RT, William Kallaghe, aliwapongeza wote waliofanikisha tukio hilo na kubainisha kwamba, kati ya malengo makuu ya shirikisho hivi sasa ni kuwekeza kwa vijana ambao ndio hazina ya kesho ya Taifa.

"Kati ya mikakati mikubwa hivi sasa ya RT ni kwenye mbio za uwanjani....Na hakuna ujanja bali kuwekeza kwa vijana na ndio maana tunawaomba na kuwahimiza wadau kusapoti katika hili.
"Vijana hawa tuliowapata ndo tunaanza nao, hivyo tunawaomba wadau mbalimbali mtuunge mkono katika hili kwa manufaa ya Taifa siku zijazo, na ambao hamkufanikiwa kuingia katika timu hii, msikate tamaa kwani bado nafasi mnayo mzidishe juhudi," alisema Kallaghe na kuongeza.

Timu hiyo itaingia kambini mapema Jumatatu kwenye hosteli za Baraza la Maaskofu (TEC), Kurasini jijini Dar es Salaam.
Wanariadha 19 waliopenya ni pamoja na Siwema Julias, Shija Donald, Salma Samwel, Christina George, Elizabeth Kirario,     Bravo George, Kimena Kibase, Damian Christian, Fedelis Amadi, Baraka Tiluli na Emmanuel Amos.

Wengine ni Elizabeth Ilanda, Gaudensia Maneno, Elia Clement, Nicodemus Joseph, Nelson Mangura, Jackson Sylvester, Dickson Mangura na Malcolm Kazmir.

RT YATEKELEZA MAAGIZO YA BMT

March 05, 2023

 

Kulia ni Makamu wa Rais wa Shirikisho la Riadha Tanzania RT , Ndugu William Kallaghe akikabidhi ripoti kwa Katibu Mkuu Mtendaji wa BMT, Bi. Neema Msitha Jijini Dar es Salaam.


SHIRIKISHO la Riadha Tanzania (RT), Machi 3, 2022, limetekeleza agizo la Baraza la Michezo la Taifa (BMT), baada ya kukabidhi ripoti ya mapato na matumizi.

Ripoti hiyo imekabidhiwa na Makamu wa Rais wa RT, William Kallaghe, kwa Katibu Mtendaji wa BMT, Neema Msitha.
BMT ilifanya kikao na Kamati ya Utendaji ya RT,    Januari 21 kwenye moja ya kumbi za Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam, na moja ya maelekezo ya Baraza, ilikuwa ni kuitaka RT kuwasilisha ripoti ya mapato na matumizi 2020/21 hadi 2021/22.

Baada ya kuipokea ripoti hiyo, Katibu Mtendaji BMT, Msitha, alisema watakaa na kuifanyia kazi.

RT YAWATAKA WATAALAM WA RIADHA NCHINI KUWASILISHA TAARIFA ZAO

February 05, 2023

 





NA TULLO CHAMBO, RT

SHIRIKISHO la Riadha Tanzania (RT), limewataka wataalamu wote wa mchezo huo kuwasilisha taarifa zinazoonyesha fani zao.
Agizo hilo, limetolewa na Kaimu Katibu Mkuu RT, Wakili Jackson Ndaweka, ambako amewataka makatibu wa vyama vya riadha mikoa yote ya Tanzania Bara, kuwajulisha wataalam wa riadha waliopo mikoani mwao, kuwasilisha taarifa zinazoonyesha fani zao katika mchezo huo. 

Wakili Ndaweka,amesema RT inakusudia kuendesha kozi mbalimbali za kuboresha uwezo wa wataalamu wa mchezo wa riadha waliopo na kuzalisha wengine katika fani ambazo zina upungufu. 

"Ili mpango huu uweze kutekelezeka kwa ufanisi, ni lazima kuwa na taarifa za wataalamu wa Riadha nchini, zitakazowezesha kuainisha maeneo yenye upungufu na kuyawekea mpango maalum," alisema na kufafanua. 

Taarifa zinazotakiwa zinapaswa kuwasilishwa kupitia wasifu 'CV', ambayo inapaswa kuambatanishwa na vivuli vya vyeti vya elimu ya Riadha na elimu ya kawaida. 

Wakili Ndaweka, alisema takwimu hizo ni muhimu sana kwa maendeleo ya mchezo wa riadha nchini. 

"Makatibu wanapaswa kuwajulisha wataalam waliopo kwenye mikoa yao, wawasilishe taarifa hizo kupitia anuani ya barua pepe ya shirikisho ambayo ni tan@mf.worldathletics.org si zaidi ya tarehe 20/02/2023," alisisitiza Ndaweka.

RT YAANIKA MATUKIO MANNE MAKUBWA YA KIMATAIFA 2023

February 04, 2023

 


| Yataka ushirikiano, uwajibikaji ngazi zote

|Timu ya Cross Country kuagwa Februari 14

NA TULLO CHAMBO, RT

SHIRIKISHO la Riadha Tanzania (RT), limeanika matukio manne makubwa ya kimataifa yanayolikabili mwaka 2023 na kusisitiza uwajibikaji wa pamoja kwa ngazi zote ili kuleta matokeo chanya.

Akizungumza na Wanahabari jijini Mwanza Februari 3, Rais wa RT, Silas Lucas Isangi, ameyataja matukio hayo ni Mashindano ya Mbio za Nyika 'Cross Country' ya Dunia, Bathurst, Australia Februari 18, Mashindano ya Vijana Afrika Mashariki (EAAR), U 18 na 20 Tanzania itakuwa mwenyeji Machi 10-11.

Tukio la tatu, Isangi alitaja ni Mashindano ya Afrika U 18 na 20 Lusaka Zambia  Aprili 27 hadi Mei 3.

"Pia kuna mashindano ya Common Wealth U 18 huko Trinidad na Tobago Agosti 4-11, vile vile All Africa Games Julai 4-23 nchini Ghana na Mashindano ya Dunia Budapest, Hungary" alisema na kuongeza.

Kwa kifupi mwaka huu uko bize sana, hivyo viongozi wa Riadha ngazi za chini kabisa, lazima wote tuamke na kutimiza wajibu kwa vitendo.

Rais Isangi, aliitaka mikoa yote ifanye mashindano ya vijana ili kufanikisha upatikanaji wa timu ya Taifa U 18 na 20 yenye tija. Pia ushiriki wao kwenye mashindano ya Taifa uwe wenye tija.

TIMU YA TAIFA CROSS COUNTRY
Rais Isangi, amesema timu hiyo imeanza kambi toka Februari Mosi katika Hoteli ya Mvono, Ngaramtoni jijini Arusha kwa gharama za shirikisho asilimia 100.

Amesema, timu itakaa kambini hadi Februari 12, itakapokwenda jijini Dar es Salaam tayari kwa kuagwa Februari 14, kabla ya kukwea pipa kwa safari ya Australia.

Amesema timu hiyo itakuwa chini ya Kiongozi wa msafara, Wakili Jackson Ndaweka ambaye ni Kaimu Katibu Mkuu RT, Kocha Denis Male, huku wachezaji ni Mathayo Sombi, Inyasi Sulle, Fabian Nelson na Josephat Gisemo.

"Maandalizi yote yamekamilika ikiwamo tiketi, visa na vibali vyote vya serikali vimekamilika," alisema na kuishukuru serikali kupitia Baraza la Michezo la Taifa (BMT), kwa kusaidia katika maandalizi hayo.

MIKOA YATAKIWA KUHAKIKISHA MASHINDANO YA RIADHA VIJANA YANAANZIA NGAZI YA WILAYA

January 27, 2023

 


Kaimu Katibu Mkuu RT, Wakili Jackson Ndaweka.

SHIRIKISHO la Riadha Tanzania (RT), limeitaka mikoa yote nchini kuhakikisha inaendesha mashindani ya Vijana chini miaka 20 na 18 'U-20 U-18' kuanzia ngazi ya Wilaya.


Maelekezo hayo yametolewa na Kaimu Katibu Mkuu RT, Wakili Msomi Jackson Ndaweka, katika barua yake ya Januari 25 kwenda kwa viongozi wa vyama vya mikoa Tanzania Bara.


Amewaelekeza viongozi hao, kukumbuka kwamba kuna jukumu kubwa mbele yao, kwani mwaka huu una mashindano mengi ya vijana wa umri huo.


 Wakili Ndaweka, aliyataja mashindano hayo kuwa ni Afrika Mashariki U-18 na 20, Tanzania ikiwa mwenyeji, ambapo awali yalikuwa yamepangwa kufanyika Kigali, Rwanda.


Alisema, mashindano hayo yatafuatiwa na ya Afrika kwa umri huo Lusaka, Zambia Aprili 27 hadi Mei 3, 2023.


"Ili kuhakikisha nchi inashiriki kwa mafanikio mashindano hayo, lazima mashindano yaanzie ngazi ya Wilaya, kisha Mkoa na mwisho mashindano ya Taifa ya Wazi kwa vijana wa umri huo ambayo yanatarajiwa kufanyika Februari 25," alisema na kuongeza.


 Mashindano ya Wilaya yafanyike kati ya Februari 9-11 na Mikoa Februari 13-19.

 

"Utaratibu huu, unakusudia kuhakikisha wanapatikana wachezaji wenye uwezo mkubwa, ili kuleta tija katika ushiriki wa nchi kwenye mashindano ya kimataifa," alisema Wakili Ndaweka. 


Sambamba na hilo, RT inakusudia na imejipanga kuhakikisha kuwa kalenda yake inafuatwa na matukio yote yanafanyika kama yalivyopangwa.

LADIES FIRST 2023 YAZIDI KUFUNGUA NEEMA RIADHA TANZANIA.

January 26, 2023


Sudan Kusini yaipa shavu RT, Simbu Balozi mpya JICA


NA TULLO CHAMBO, RT


MASHINDANO Maalum ya Riadha ya Wanawake nchini Tanzania maarufu kama Ladies First, yamezidi kufungua ushirikiano wa mchezo huo kimataifa.


Ladies First ikiwa ni wazo la Nguli wa Riadha nchini Tanzania, Kanali mstaafu Juma Ikangaa, imefanyika mwaka huu ukiwa ni msimu wa nne na kushirikisha mikoa 30 Kati ya 31 Tanzania Bara na Visiwani.


Mwaka huu, mashindano hayo yalifanyika January 21 na 22 kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam na kushirikisha zaidi ya wanariadha 186.


Kanali Mstaafu Ikangaa, ambaye enzi zake aliiwakilisha vema Tanzania kimataifa katika mbio za marathoni, ikiwemo nchini Japan, nchi hiyo imekuwa ikimuenzi na kumpa heshima kubwa ambapo hivi sasa ni Balozi wa Hiari wa Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Japan (JICA).


Katika kumuenzi Kanali Ikangaa, Japan ilimtaka kusema kitu ambacho nchi hiyo iifanyie Tanzania, ndipo kwa kushirikiana na wadau wake mbalimbali, akaja na wazo la kuwaenzi na kuhamasisha wanawake kushiriki katika mchezo wa Riadha, hasa ikizingatiwa medali ya kwanza ya kimataifa Tanzania ililetwa na Mwanamke Theresia Dismas mwaka 1964, katika michezo ya All Africa nchini Congo Brazzaville, kupitia mchezo wa Kurusha Mkuki 'Javelin'.


Wazo hilo lilianza kutekelezeka mwaka 2017 kwa mashindano yaliyofanyika Uwanja wa Taifa, sasa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam, ambapo baadhi ya washindi wamekuwa wakipata nafasi ya kwenda kushiriki mbio za Nagai City nchini Japan.

Katibu Mtendaji wa Baraza la Michezo la Taifa Tanzania (BMT), Bi. Neema Msitha, aliipongeza JICA na kampuni mbalimbali za Kijapan zinazofanya kazi nchini, Kanali Ikangaa,serikali ya Tanzania na Shirikisho la Riadha Tanzania (RT), kwa kufanikisha mashindano hayo kwa msimu wa nne sasa.


Bi. Msitha, anasema mashindano hayo yalianza mwaka 2017 na kufanyika kwa mafanikio makubwa miaka mitatu mfululizo hadi 2019 kabla kusitishwa kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo janga la UVIKO 19 'Covid 19'.


"Lengo la mashindano haya ni kuhamasisha ushiriki wa watoto wa kike katika michezo hususan Riadha, kutoa fursa kwa wanariadha wa kike kuonyesha vipaji vyao na kuendeleza vipaji vya wanariadha ambao wataiwakilisha nchi katika mashindano ya kitaifa na kimataifa," anasema Bi. Msitha.


Tangu kuanza kwa mashindano hayo mwaka 2017, Wanariadha wa Tanzania na viongozi wao, wamekuwa wakipata nafasi ya kwenda kushiriki Nagai Marathon, ambapo wanariadha akiwemo Angel John Joseph Yumba, Fabian Nelson Sulle, Fabian Joseph, Alphonce Felix Simbu na wengineo wameweza kung'ara.


Mbali na hilo, Ladies First iliweza kuishirikisha nchi ya Sudan Kusini na kushiriki mashindano ya mwaka 2019 jijini Dar es Salaam.


Mwaka huu 2023, Ladies First imezidi kufungua milango katika mchezo wa Riadha Tanzania, ambapo Sudan Kusini iliwakilishwa na viongozi wake mbalimbali akiwemo Katibu Mkuu wa Wizara ya Michezo nchini humo, Peter Baptist, Balozi wa nchi hiyo nchini Tanzania, Deng Abel na wengineo.

Baptist katika salamu zake, mbali na kushukuru na kupongeza Tanzania kwa mashindano hayo, anasema na kwao wana mashindano kama hayo yajulikanayo kama 'Umoja na Amani', yakilenga kutumia michezo kuhamasisha amani na umoja katika Taifa hilo ambalo liliandamwa na vita miongoni mwao kwa miaka kadhaa.


Mwakilishi huyo, anasema katika kuendeleza ushirikiano na Tanzania, wanatoa mwaliko kwa wanariadha wanne waliofanya vizuri katika Ladies First 2023 wa mbio tofauti ukiondoa mita 5000 kwenda Sudan Kusini kushiriki mashindano hayo yanayotarajiwa kufanyika miezi miwili ijayo.


Mbali na fursa hizo zilizojitokeza Ladies First 2023, nyingine ni kwa Mwanariadha anayefanya vema hivi sasa, Mshindi wa Medali ya Fedha Common Wealth Games 2022, Alphonce Simbu, naye kuteuliwa kuwa Balozi wa Hiari JICA, akiungana na Kanali mstaafu Ikangaa.


Haya ni kati ya mafanikio ya Ladies First 2023, na hakika uwajibikaji ukizidi kuongezeka, bila shaka milango zaidi itazidi kufunguka katika medani ya riadha Tanzania.

Gwajima Anogesha Ufunguzi wa LADIES FIRST Dimba la Benjamin Mkapa, Dar es Salaam

January 22, 2023
Waziri Dkt. Dorothy Gwajima wa pili kutoka Kulia, akishiriki Maoezi ya Viungo wakati wa ufunguzi wa Mashindano ya Ladies First kwa msimu wa Nne, wa kwanza kutoka kulia ni Mwenyekiti wa BMT, Leodegar Tenga, Balozi wa Japan Tanzania kushoto kwa Waziri, na Katibu Mtendaji wa BMT, Neema Y. Msitha 


 NA TULLO CHAMBO - AT


MSIMU wa Nne wa Mashindano ya Riadha ya Wanawake maarufu kama 'Ladies First' umefunguliwa kwa kishindo kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam Januari 21 na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Dorothy  Gwajima.

Mashindano hayo  ya siku mbili yameandaliwa na Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Japan (JICA), kwa kushirikiana na  Shirikisho la Riadha Tanzania (RT).
 
Ufunguzi huo, ulipambwa na vikundi mbalimbali vya Jogging, burudani mbalimbali akiwamo Msanii maarufu wa Singeli, Dullah Makabila, aliyepagawisha vilivyo na wanariadha wa kike.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Dkt. Gwajima, alisema wataendelea kuwekeza kwa watoto ngazi ya vijiji ili kuibua vipaji vipya, ambavyo vitapata fursa ya kushiriki mashindano mbalimbali kitaifa na kimataifa siku za mbeleni.

Pia, alisema watahakikisha wanasuka upya mikakati katika shule mbalimbali ili kupata muonekano mpya katika michezo.

"Nitoe wito kwa wazazi kutoa fursa kwa vijana wao wa kike, kujitokeza kushiriki michezo kwani ni ajira itakayosaidia kujikwamua kiuchumi katika familia zao," alisema Dkt. Gwajima.

Kwa upande wake, Katibu Mtendaji wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Neema Msitha, alisema lengo kubwa la mashindano hayo ni kuhamasisha watoto wa kike kushiriki katika michezo, kwani michezo ni fursa na ajira.

Aliwapongeza JICA kwa kufanikisha kwa kiasi kikubwa Mashindano hayo, RT, vyama vya Riadha vya Mikoa, Makatibu Tawala wa Mikoa kwa kuwezesha wachezaji wao kufika Dar es Salaam kwa ajili ya mashindano hayo, Ofisi ya Mkurugenzi Manispaa ya Temeke kwa kuruhusu zaidi ya wanafunzi 1,000 kuhudhuria mashindano hayo na kujifunza, na Mwanariadha mahiri wa zamani, Kanali Mstaafu Juma Ikangaa, ambaye pia ni Balozi wa Hiari wa JICA, kwa kuasisi wazo la kuanzishwa mashindano hayo.

Balozi mwingine wa hiari wa JICA, Mwanariadha mshindi wa medali ya Fedha Jumuiya ya Madola, Alphonce Felix  Simbu, aliwataka wanariadha wa kike hao watumie fursa hiyo kujituma na kurejesha enzi za Mwanamama Theresia Dismas, ambaye ni mchezaji wa kwanza kuipa Tanzania medali ya kimataifa katika michuano ya All African Games 1965 Congo Brazaville.

Simbu, alisema kuwa ushiriki huo utakuwa chachu ya kujifikiria namna ya  Theresia Dismas alieweza kupata medali.

Kwa upande wake, Kaimu Katibu Mkuu RT, Wakili Jackson Ndaweka, aliishukuru Serikali kwa kuwezesha kupata muungano na JICA kwa kudhamini Riadha hususani kwa wanawake.
Àlisema kuwa wanawake wanatakiwa kutumia fursa ya kujiendeleza  ,kwani mahitaji kuleta ushindani . 

Mashindano hayo yatakayofikia tamati Januari 22, yanashirikisha wanariadha zaidi ya 186 kutoka mikoa yote Tanzania Bara na Visiwani.

Uzinduzi huo, pia ulihudhuriwa na Balozi wa Japan nchini Tanzania, viongozi kutoka Wizara ya Michezo Sudan Kusini, Naibu Meya Jiji la Nagai Japan, Mwenyekiti wa BMT Leodegar C. Tenga na Makamu wa Rais RT, William Kallaghe.

Kumekucha Ladies First 2023, Wanawake Kuchuana DAR

January 20, 2023


NA TULLO CHAMBO


WAZIRI wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dr. Dorothy Gwajima, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika uzinduzi wa Mashindano Maalum ya Riadha ya Wanawake maarufu kama 'Ladies First' yanayotarajiwa kurindima kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa January 21 na 22 jijini Dar es Salaam.


Akizungumza na Waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam, Katibu Mtendaji wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Neema Msitha, alisema mashindano hayo yamendaliwa na BMT, Shirikisho la Riadha Tanzania (RT), na kuwezeshwa na Shirika la Maendeleo la Japan ( JICA), na huu ni msimu wake wa nne,  yakiwa na lengo la kuwahamasisha wanawake kushiriki katika mchezo wa Riadha.


"Lengo la mashindano haya ni kuwahasisha  watoto wa kike kushiriki katika michezo hususan Riadha, kutoa fursa ya wanariadha wa like kuonyesha vipaji vyao na kuendeleza vipaji vya wanariadha ambao watawakilisha nchi katika mashindano ya kitaifa na kimataifa siku zijazo," alisema Msitha.


Alisema mashindano ya mwaka huu, yatashirikisha wanariadha 186 kutoka mikoa yote ya Tanzania Bara na Visiwani yakishirikisha mbio za Mira 100, 200, 400, 800, 1500, 5000, 10000, Kupokezana Vijiti 4x400 na Kurusha Mkuki na kushuhudiwa na watazamaji mbalimbali wakiwemo wanafunzi 1000 kutoka shule za Msingi na Sekondari za Manispaa ya Temeke.


"BMT inaishukuru Sana JICA na kampuni za Kijapan zinazofanya shughuli zake hapa nchini kwa kufadhili mashindano haya kwa mara ya  nne, pia Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kutoa uwanja ambao utatumika kwa mshindano na ofisi ya Mkurugenzi wa Manispaa ya Temeke ambayo imetoa ruhusa kwa wanafunzi kushiriki na kujifunza katika mashindano haya," alisema Msitha na kuongeza.


Baraza linaendelea kusisitiza Kamati za Michezo za Mikoa, kuhakikisha zunawezesha ushiriki wa wanaridha wa mikoa yao katika mashindano haya na kuwaomba wananchi wote wa Jiji la Dar es Salaam  kujitokeza kwa wingi siku ya Jumamosi na Jumapili kushuhudia mashindano hayo ambapo hakuna kiingilio.


Kwa upande wake, Mwakilishi Mkuu wa JICA Tanzania, Naofumi Yamura, alisema wanajivunia kuanza kutoa ushirikiano kwa Tanzania toka mwaka 1962 na mashindano ya mwaka huu watayatumia kama maadhimisho ya miaka 60 ya ushirikiano wao na Tanzania.


Yamura, alisema mashindano ya mwaka huu yatahudhuriwa na watu mbalimbali maarufu akiwemo Balozi wa Japan Tanzania, viongozi kutoka Sudan ya Kusini, Mwanariadha nguli Kanali mstaafu Juma Ikangaa na mwanariadha anayewika hivi sasa Alphonce Simbu.


Naye Katibu wa Chama cha Riadha Zanzibar (ZAAA), Muhidin Masunzu akimwakilisha Kaimu Katibu Mkuu wa RT, Wakili Jackson Ndaweka, alisema wamejiandaa vema kuhakikisha mashindano hayo yanafanyika kwa ufanisi.


Wazo la kuanzishwa mashindano hayo liliasisiwa na Kanali Ikangaa, ambaye pia no Balozi wa Hiari wa JICA, likitokana na kuenzi historia ambapo medali ya kwanza Tanzania kimataifa ililetwa na Mwanamama Thereza Dismas, aliyekuwa akirusha Mkuki.

 

Copyright © 2015 - 2025 Athletics Tanzania All Right Reserved

Developed by Gadiola Emanuel
Theme By AP | Developed By Gadiola Emanuel